Haki za mtoto – Mtoto ni nani?

Mtoto ni mtu yeyote mwenye umri wa chini ya miaka kumi na nane (18). Tafsiri hii imetokana na Mkataba wa Kimataifa wa Haki za Mtoto, Mkataba wa Afrika kuhusu Haki na Ustawi wa Mtoto, Sera ya Maendeleo ya Mtoto na Sheria ya Mtoto Na. 21 ya 2009. Katika umri huu mtoto anahitaji malezi bora ili aweze kuishi vizuri, kushirikishwa, kulindwa na kuendelezwa kiakili kwa ajili ya maisha yake ya baadae ya utu uzima.

Haki za mtoto

Watoto wana haki za kipekee kwa sababu umri wao mdogo na hali ya utegemezi vinaweza kuwafanya wadhulumiwe na kutendewa vitendo vibaya. Watoto wote wana haki sawa bila kujali jinsia, rangi, kabila, dini, hadhi au hali ya afya. Umoja wa mataifa, Serikali, wazazi/walezi na jamii kwa ujumla wana wajibu wa kuhakikisha watoto wanapatiwa haki zao. Haki za mtoto zimegawanyika katika makundi makuu manne (4) yafuatayo:

  • Haki ya Kuishi: Inahusu kulinda na kuendeleza uhai wa mtoto ikiwepo:
    • Kuzuia magonjwa na kupata huduma za matibabu,
    • Chanjo na kufuatilia ukuaji
    • Lishe bora
    • Mavazi yanayositiri
    • Makazi salama
    • Maji safi na salama
    • Usafi wa aina zote
  • Haki ya Kuendelezwa: Maendeleo ya mtoto kiakili ikijumuisha:
    • Elimu (rasmi na isiyo rasmi)
    • Tamaduni, mila na desturi sahihi za jamii yake.
    • Kiroho
    • Vipaji
  • Haki ya kulindwa: Kuhakikisha mtoto analindwa dhidi ya:
    • Unyanyaswaji na ubaguzi
    • Ukatili (kimwili, kingono na kihisia)
    • Unyonywaji ikiwa ni pamoja na ajira za utotoni
    • Ukeketaji, ndoa za utotoni, ukatili wa kijinsia
    • Mazingira hatarishi
    • Kutelekezwa au kuachwa bila mlezi
  • Haki ya kushiriki

Haki za mtoto

Kundi hili linahakikisha kwamba watoto wanapatiwa nafasi ya kutoa mawazo na kwamba maoni yao yanazingatiwa hasa katika maamuzi yanayo athiri maisha yao. Mtoto anapaswa kushirikishwa katika ngazi zote zote kuanzia kwenye familia, jamii na taifa. Wajibu wa wazazi/jamii katika kuhakikisha watoto wanapatiwa haki zao

  1. Wazazi/walezi wana wajibu wa kuwahudumia watoto wao na kuhakikisha wanapata mahitaji yao ya msingi.
  2. Kuhakikisha kwamba watoto wanalindwa dhidi ya magonjwa, wanapelekwa kwenye chanjo, wanapatiwa huduma za afya na lishe bora.
  3. Kuwaandikisha shule, kufuatilia maendeleo yao shuleni na kuwapatia mahitaji yote ya shule.
  4. Watoto wanashirikishwa, kuongozwa na kuhakikisha watoto wanatimiza wajibu wao kikamilifu ikiwa ni pamoja na kufuata imani, tamaduni sahihi, kuzingatia masomo, kujilinda, kujifunza na kusaidia kazi za nyumbani zisizo athiri elimu, afya na zinazoendana na uwezo wa mtoto.
  5. Kulinda watoto dhidi ya kunyanyaswa, unyonywaji, kutelekezwa, kufanyiwa ukatili na kuchukua hatua pale ambapo haki za mtoto zimevunjwa.
  6. Kushirikiana na serikali na wadau wengine katika kuhakikisha huduma zinapatikana kwa viwango stahiki katika maeneo yao.

Vyanzo

www.wvi.org/tanzania

Shares:
Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *