Maelezo ya jumla

Kichaa cha mbwa (Rabies) ni ugonjwa hatari sana wa wanyama unaosababishwa na virusi. Unaweza kuwapata wanyama wa mwitu, kama vile kicheche, popo na mbweha. Unaweza pia kuwapata wanyama wa nyumbani kama mbwa, paka au wanyama wengine. Watu hupata ugonjwa huu baada ya kuumwa na mnyama aliyeambukizwa.

Je! Nini dalili za kichaa cha mbwa?

Wagonjwa wengi huugua baada ya kuumwa na mnyama ambaye anahisiwa kuwa na kichaa cha mbwa. Anaweza kuwa mnyama wa kufugwa au mnyama wa mwituni. Dalili za kichaa cha mbwa hutokana na virusi wanaosababisha ugonjwa kuvamia na kusababisha kuvimba kwa ubongo (encephalitis). Baada ya maambukizi, mgonjwa anaweza kukaa muda mfupi tu na kuanza kuona dalili, au, dalili zinaweza kuchelewa sana hata kwa miezi 1-3.
Ugonjwa huu hushambulia mwili haraka sana, mgonjwa huanza na dalili za kawaida zisizo maalumu kama vile homa, kutapika, kuharisha, uchovu n.k. Kisha virusi wanapoanza kushambulia mfumo wa neva, mgonjwa huanza kuonekana mwenye wasiwasi mwingi, mgomvi, hulegea sana, hupooza na dalili nyingine zinazotokana na kuvimba ubongo kama vile: Kushindwa kumeza maji kunakosababishwa na kukaza kwa misuli ya shingo- hii husababisha mgonjwa kuyaogopa maji, degedege inaweza kutokea , kisha mgonjwa huingia kwenye koma na hatimaye kifo. Baada ya dalili kuanza, karibu asilimia 100 ya wagonjwa hufa baada ya siku 7-14  hata kama watatibiwa.

Kichaa cha mbwa husababishwa na nini?

Ugonjwa huu unaweza kuwapata wanyama wa mwitu, kama vile kicheche, popo na mbweha. Unaweza pia kuwapata wanyama wa nyumbani kama mbwa, paka au wanyama wengine. Watu hupata ugonjwa huu baada ya kuumwa na mnyama aliyeambukizwa virusi vinavyosababisha kichaa cha mbwa (rabies virus).

Nani aliye kwenye hatari zaidi ya kupata kichaa cha mbwa?

Watu wanaofanya kazi au kuishi karibu na wanyama wa mwitu, kama vile kicheche, popo na mbweha, au wanaokaa na mbwa, paka au wanyama wengine wa shamba, wako kwenye hatari zaidi ya kupata ugonjwa huu. Watu hupata ugonjwa huu baada ya kuumwa na mnyama aliyeambukizwa.

Wakati gani utafute matibabu ya haraka?

Kama umeumwa na mbwa mwone mtoa huduma ya afya mapema iwezekanavyo.

Utambuzi wa kichaa cha mbwa

Utambuzi si mgumu sana kwa mgonjwa mwenye historia ya kuumwa na mnyama mwenye ugonjwa huu. Lakini mara nyingi hili huwa si rahisi, hasa kwa sababu mtu anaweza kuwa amesahau kuwa aliumwa na mbwa baada ya kukaa siku nyingi bila dalili kujitokeza. Dalili za kichaa cha mbwa hufanana sana na dalili za maambukizi mengine yanayosababisha kuvimba kwa ubongo (encephalitis). Hata hivyo,ili kufanya u

tambuzi wa uhakika daktari anaweza kuchukua tishu kutoka sehemu kadhaa za mwili kwa ajili ya vipimo, na hii hutegemea anataka kufanya kipimo cha aina gani.

  • Anaweza kuchukua tishu ya ngozi kwenye sehemu ya nyuma ya shingo –tishu hii hupimwa kuona kama kuna antijeni za kichaa cha mbwa kwa kutumia kingamwili (antibody) maalumu inayoweza kuweka mjibizo ”react” na antijeni hizo – nuchal biopsy
  • Daktari bingwa wa macho (ophtamologist) anaweza kuchukua sampli jichoni kwa ajili ya kupima (kama ilivyofanyika hapo juu)
  • Daktari anaweza kuchukua Mate, ute (CSF) toka kwenye uti wa mgongo au tishu ya ubongo (mara nyingi hii hufanyika mtu akishakufa) kwa ajili ya kuvipima.-Viral cultures and polymerase chain reaction

Vipimo hivi vyote hufanyika katika maabara maalumu, kwa hiyo, sampuli hizi zitapaswa kusafirishwa kwenda katika maabara maalumu yenye uwezo wa kutambua ugonjwa huu.

Uchaguzi wa matibabu

Hakuna tiba ya kuponya ugonjwa huu baada ya dalili kuanza, lakini kupona kwa mtu mmoja, japo kwa nadra sana, kunatoa matumaini kuwa tiba inaweza kupatikana hivi karibuni.
Kwa mwanadamu, dalili za ugonjwa huu ni pamoja na homa, kichwa kuuma na uchovu, kisha wendawazimu, na kupooza. Mara baada ya dalili kuaanza mgonjwa huwa hawezi kupona tena- atakufa.
Kwa watu walioumwa na mbwa mwenye kichaa, wanaweza kukingwa wasipate kichaa cha umbwa kwa kuchoma sindano mfululizo za chanjo siku ya 0, 3, 7, 14, and 28. Unapaswa kuchomwa chanjo hizi mara moja. Ukiumwa na mnyama, osha kidonda vyma na maji safi kisha fika hosipitali kwa ajili ya matibabu.

Nini cha kutarajia?

Hakuna tiba ya kuponya ugonjwa huu baada ya dalili kuanza, lakini kupona kwa mtu mmoja, japo kwa nadra sana, kunatoa matumaini kuwa tiba inaweza kupatikana hivi karibuni.

Matatizo yanayoweza kutokea

Maambukizi kwenye ubongo na uti wa mgongo na kifo.

Kuzuia

Kuzuia kichaa cha mbwa fanya yafuatayo

  • Wapatie chanjo wanyama wako wa kufugwa. Chanjo za kichaa cha mbwa zipo kwa jili ya mbwa, paka na wanyama wote wa shamba.
  • Usiwaache wanayama wako wa kufugwa kuzurura zurura mitaani
  • Usiwakaribie wanyama wanaotangatanga mtaani. Mnyama mwenye kichaa cha mbwa anaweza kuwa mkali na mgomvi au anaweza kuonekana mchovu na mnyong’ofu.

MAELEZO ZAIDI KUHUSU UGONJWA WA KICHAA CHA MBWA

Maelezo ya jumla

Ni ugonjwa ambao karibu mar azote unasababisha kifo; unashambulia ubongo na utando unaofunika uti wa mgongo na ubongo.

Sababu ya kichaa cha mbwa

Rabies virus

Epidemiolojia ya kichaa cha mbwa

Ulimwenguni kote, hasa katika nchi zinazoendelea. Kwa kawaida huu ni ugonjwa wa wanyama. Ugonjwa huu unaambukizwa kwa kung’atwa.

Uambukizo wa kichaa cha mbwa

Unaambukizwa kupitia mate ya mnyama mwenye kichaa cha mbwa anapokuuma au kukwaruza. Maambukizi kutoka kwa mwanadamu mmoja mpaka mwingine kunawezekana kinadharia, lakini hakuna kisa kilichowahi kurekodiwa.

Muda kabla dalili kuanza

Kwa kawaida ni wiki 3-8

Muda wa uambukizo

Kwa kawaida ni siku 3-7 kabla ya dalili za ugonjwa kuanza kuonekana na mnyama anaendelea kuwa na uwezo wa kuambukiza kipindi chote cha maisha yake

Nani yuko kwenye hatari

Wanyama wote wako kwenye hatari kwa viwango tofauti.

Dalili za kichaa cha mbwa

Dalili za ugonjwa kwa wanyama wote, ikiwemo na mwandamu, zinatokea katka hatua tatu;

  • Hatua ya 1 – prodromal phase
  • Hatua ya 2 – excitatory phase
  • Hatua ya 3 – paralytic phase

Hatua ya kwanza: Dalili zinaanza na mtu kuanza kujihisi/kuogopa kuwa kitu kibaya kinakwenda kutokea, maumivu ya kichwa, homa na kichefuchefu, kujisikia vibaya sehemu ya kidonda ulipoumwa (panaweza kuwasha au kupata ganzi)

Hatua ya pili: Sauti kidogo/ upepo unamshtua mgonjwa, anakuwa mkali, asiyetulia, anaonekana mwoga sana, anauma watu, ni baadhi ya dalili

Hatua ya tatu: Kukakamaa kwa misuli inayosaidia kumeza kunasababisha kutokwa mate na kuogopa maji. Kuchanganyikiwa na degedege na kifo kinatokea kwa sababu ya kushindwa kupumua.

Utambuzi wa kichaa cha mbwa

Kuwepo kwa historia ya kuumwa na mnyama mwenye kichaa cha mbwa na anaonesha dalili

Matibabu

  1. Kuhudumia kidonda
  • Osha vizuri kidonda kwa maji na sabuni ili kupunguza virusi
  • Kama kidonda kinavuja damu kifunike
  • Kamwe usishone kidonda maana utasababisha virusi kusambaa zaidi
  1. Mpatie mgonjwa chanjo ya kichaa cha mbwa haraka kama imehakikiwa kuwa mnyama anaumwa

Kuzuia kichaa cha mbwa

  1. Patia chanjo mbwa na paka wote
  2. Wakamate na wafungie mbwa na paka wote wanaonekana wana afya njema kwa siku 10 wameng’ata watu
  3. Toa matibabu baada ya kung’atwa
    • Tibu sehemu ya kidonda
    • Toa chanjo – immunogic protection
  1. Waache mbwa na paka nyumbani.
  2. Ua paka na mbwa koko wote katika maeneo yenye mlipuko wa kichaa cha mbwa

Vyanzo

http://wwwnc.cdc.gov/travel/yellowbook/2012/chapter-3-infectious-diseases-related-to-travel/rabies.htm

Shares:
2 Comments
  • Rajabu zahoro sangaga
    Rajabu zahoro sangaga
    March 31, 2021 at 8:53 am

    “Kama ukiwa unamuuguza mgonjwa wa kichaa cha mbwa, na ikatokea akakung’ata au kukukwarua kwa makucha, je Kuna uwezekano wa kupata maambukizi. “

    Reply
    • Dr.Mniko
      Dr.Mniko
      March 31, 2021 at 6:41 pm

      Ndio unaweza kupata maambukizi, kama ilivyo kwa mbwa , virusi wanaosababisha kichaa cha mbwa hukaa pia kwenye mate ya mtu mwenye ugonjwa huu
      Kama akikung’ata utaugua poa

      Reply
Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *