Maelezo ya jumla
Kidondamalazi (Bedsore) ni kidonda kinachotokea kwenye ngozi baada ya shinikizo la muda mrefu linalotokana na kutokujongea kwa muda mrefu (mf: Kuketi au kulala kwa muda mrefu bila kujongea). Kidondamalazi huwapata wagonjwa waliolazwa kitandani kwa muda mrefu sana.
Je! Nini dalili za kidondamalazi?
Dalili za kidondamalazi zimegawanywa katika hatua nne, kila moja ikielezea ukali wake. Hatua I (ishara za kwanza) na hatua ya nne (ishara mbaya zaidi):
- Hatua ya I: Kuna eneo jekundu kwenye ngozi ambalo ukilibonyeza halibadiliki na kuwa jeupe, hii ni ishara ya mwanzo kuwa kidonda kinaanza kutengenezeka.
- Hatua Ya II: Ngozi hutengeneza malengelenge ambayo baadae hupasuka na kusababisha kidonda. Kuna wekundu kwenye eneo linalozunguka kidonda na linawasha.
- Hatua ya III: Ngozi hubanduka kabisa na kidonda huanza kuchimbika na kuharibu tishu zinazofunikwa na ngozi.
- Hatua ya IV: Katika hatua hii, huwa kidonda kimechimbika sana mpaka kimeharibu misuli,mifupa na hata kano (tendons) na viungo (joints).
Nani yuko kwenye hatari zaidi ya kidondamalazi?
Watu walio katika hatari zaidi ya kupata kidondamalazi ni pamoja na:
- Watu waliolazwa kitandani kwa muda mrefu
- Walemavu wanaotumia kiti cha magurudumu
- Utapia mlo
- Hatari huongezeka kadri umri unavyoongezeka
- Watu wenye jeraha au ugonjwa unaopunguza uwezo wao wa kujongea (mfano: kuumia mgongo)
- Watu wenye hali/ugonjwa unaoweza kuzuia damu kufika sehemu fulani za mwili (mfano: kisukari)
- Watu wenye ugonjwa unaosababisha kushindwa kuzuia kinyesi au mkojo, wanajinyea au kujikojolea
- Watu wenye ugonjwa wa akili unaosababisha washindwe kutembea (mf; Alzheimer’s)
Wakati gani utafute matibabu ya haraka?
Mwone mtoa hudumaa ya afya kama eneo lina malengelenge au kidonda. Kama kuna dalili za maambukizi kwenye kidonda mwone haraka mtoa huduma ya afya. Maambukizi yanaweza kuenea mwili mzima na kusababisha matatizo makubwa zaidi.
Ishara za maambuzi ni pamoja na:
- Harufu mbaya kutoka kwenye kidonda
- Wekundu na maumivu karibu na kidonda
- Joto na kuvimba kwa ngozi inayozunguka kidonda
Homa, uchovu, na kuchanganyikiwa ni ishara kwamba maambukizi yameenea kwenye damu na mahali pengine mwilini.
Utambuzi
Kidondamalazi si tofauti na vidonda vingine. Mara nyingi historia ya mgonjwa huchangia sana katika utambuzi.
Uchaguzi wa matibabu
Kama ikigundulika kuna kidondamalazi,hatua zifuatazo zinaweza kuchukuliwa mara moja:
- Jaribu kupunguza shinikizo katika eneo lenye kidonda kwa kutumia mito au takia (cushion)
- Kidondamalazi kitatibiwa kulingana na hatua yake, mtoa huduma ya afya atakupa matibabu kulingana na hatua ya kidondamalazi..
- Jaribu kuepuka kusugua eneo lenye kidonda. Unaweza pia kutia powder maalumu kwenye shuka ili kupunguza msuguano. (kuna bidhaa zilizotengenezwa maalumu kwa ajili ya tatizo hili, ulizia kwenye maduka ya dawa)
- Boresha lishe na tibu matatizo mengine yanayochelewesha kidonda kupona.
- Kama kidonda kiko katika hatua ya II au zaidi, mtoa huduma atakupa maagizo jinsi ya kukisafisha na kukitunza. Ni muhimu sana kusafisha kidonda vyema ili kuzuia maambukizi.
- Hakikisha eneo lenye kidonda ni safi kila wakati. Ondoa tishu zilizokufa kwa kumwagia maji masafi yenye chumvi kidogo. Kidonda kinapaswa kufunikwa vyema kwa dressing gauze ya kufungia vidondamalazi.