Maelezo ya jumla

Kikojozi ”bedwetter” ni mtoto wa miaka 5 mpaka 6 anayejikojolea bila hiari yake – ana tatizo la kukojoa kitandani. Anaweza kujikojolewa wakati wowote ,iwe usiku au mchana. Makala hii inalenga kuzungumzia zaidi kujikojolea wakati wa usiku.

Kikojozi ni nani ?

Dalili kuu ni kukojoa bila hiari ,hasa wakati wa usiku, na hutokea angalau mara mbili kwa mwezi.

Kukojoa kitandani usiku husababishwa na nini?kikojozi

  • Kila mtoto huacha kuwa kikojozi katika umri tofauti. Mara nyingi kuacha kukojoa kitandani usiku ni hatua ya mwisho kabisa ya kujifunza kutumia choo. Watoto wa miaka 5,6 au zaidi wanapokojoa kitandani huitwa vikojozi.
  • Kukojoa kitandani usiku ni jambo la kawaida. Watoto zaidi ya milioni 5 nchini Marekani wanakojoa kitandani usiku (Tanzania hatuna takwimu za kufaa).
  • Watoto ambao waliacha kukojoa kitandani kwa takribani miezi sita au zaidi na kisha wakaanza tena kukojoa wana ”secondary enuresis”. Kuna sababu nyingi za mtoto kuanza kukojoa tena baada ya kuwa mkavu kwa kitambo. Sababu inaweza kuwa ya kimwili, kihisia, au mabadiliko ya muda wa kulala.
  • Watoto ambao hawajawahi kuacha kabisa kukojoa kitandani usiku wana primary enuresis. Hii mara nyingi hutokea kwa sababu, mwili hutengeneza mkojo mwingi zaidi kuliko uwezo wa kibofu na mtoto haamki kibofu kinapojaa. Ubongo wa mtoto bado haujajifunza kuitikia ishara kwamba kibofu kimejaa. Hili si kosa la mtoto au mzazi.
  • Sababu za kimwili ni chache, lakini zinaweza kujumuisha vidonda/tatizo kwenye uti wa mgongo, Matatizo ya kuzaliwa nayo ya mfumo wa mkojo, maambukizi kwenye mfumo wa mkojo na kisukari.
  • Kukojoa kitandani ni tatizo linalorithiwa kwenye familia.
  • Takribani wavulana 9% na wasichana 6% wenye umri wa miaka saba hukojoa kitandani. Idadi hii hupungua kidogo wanapofikia umri wa miaka 10. Ijapokuwa tatizo hili huondoka lenyewe kadri umri unapoongezeka, kuna watu kadhaa huwa vikojozi hadi utu uzima.

Mwanao akiwa kikojozi ni wakati gani utafute matibabu ya haraka?

Utambuzi wa tatizo la kukojoa kitandani

  • Daktari atauliza historia ya kukojoa kitandani ya mtoto. Unaweza kusaidia kwa kutunza kumbukumbu kwenye daftari ,andika amekojoa mara ngapi kwa siku, saa ngapi, vinywaji alivyokunywa, chakula alichokula na muda aliolala.
  • Uchunguzi wa mwili unapaswa kufanyika ili kuhakikisha hakuna sababu za kimwili zinazosababisha.
  • Urinalysis (kipimo cha mkojo) itafanyika ili kuhakikisha hakuna maambukizi kwenye njia ya mkojo au
  • Eksirei ya figo, kibofu na vipimo vingine havihitajiki, labda kama kuna tatizo lingine.

Uchaguzi wa matibabu kama mwanao ni kikojozi

  • Kila mmoja hupokea swala hili kwa hisia tofauti, watu wengine huchukulia poa na wengine humuadhibu mtoto. Mambo haya yote hayasaidii kupunguza tatizo. Unatakiwa kumhakikishia mtoto wako kuwa kukojoa kitandani ni jambo la kawaida na linaweza kushughulikiwa.
  • Anza kwa kuhakikisha mtoto wako anakojoa kila mara wakati wa mchana na jioni ili asikae na mkojo kwa muda mrefu. Hakikisha mtoto anakojoa kabla ya kwenda kulala. Unaweza pia kupunguza kiasi cha vinywaji anavyokunywa masaa machache kabla ya kulala. KUMBUKA KUWA unapaswa kupunguza kiasi na sio kumnyima kabisa mtoto vinywaji.
  • Mpe zawadi mtoto kwa kila usiku asiokojoa kitandani. Baadhi ya familia hutunza daftari analojaza mtoto kila asubuhi anapoamka mkavu bila kukojoa kitandani. Njia hii sio ya uhakika kwamba itaondoa tatizo, lakini unaweza kuijaribu kabla haujafikiria kuanza kutumia madawa. Njia hii inawafaa zaidi watoto wadogo wa umri kati ya miaka 5 hadi 8.
  • Desmopressin ni dawa inayotumika kutibu ukojozi. Inapunguza kiasi cha mkojo kinachotengenezwa wakati wa usiku. Ni rahisi sana kutumia desmopressin na hutoa matokeo ya haraka. Inaweza kutumika kwa muda mfupi, hasa mtoto anapokuwa ugenini au anapopata mgeni chumbani kwake, au kwa matumizi ya muda mrefu. Daktari anaweza kupendekeza kuacha kutumia dawa hii kwa nyakati fulani fulani ili kuona kama mtoto anaweza kubaki mkavu bila dawa.
  • Tricyclic antidepressants (mara nyingi imipramine) – dawa hizi zinaweza pia kusaidia kupunguza ukojozi. Lakini madhara yake yanaweza kukera na kutumia kiwango kikubwa cha dawa hii kinaweza kutishia maisha ya mtoto. Kwa hiyo, madawa haya hutumiwa pale tu matibabu mengine yanapokuwa yameshindwa kabisa.
  • Kwa watoto ambao wamekuwa wakavu kwa takribani miezi sita kisha wakaanza kukojoa tena (secondary enuresis), daktari atatafuta sababu ya kuanza kujikojolea tena, kisha atakupatia mapendekezo ya tiba.

Nini cha kutarajia kama mwanao ni kikojozi?

  • Kama hakuna tatizo la kimwili, hali hii haimdhuru mtoto kiafya.
  • Kwa sababu ya tatizo hili mtoto anaweza kujisikia aibu au hata kuanza kutokujiamini. Ni muhimu kumtia moyo mtoto na si kumkerehesha zaidi.
  • Watoto wengi, huwa sawa baada ya njia mojawapo ya matibabu kutumika.

Matatizo yanayoweza kutokea kama una tataizo la kukojoa kitandani

  • Matatizo yanaweza kutokea kama kuna tatizo la kimwili linalosababisha hali hii na halishughulikiwi.
  • Matatizo ya kisaikolojia yanaweza kutokea kama tatizo hili halitashughulikiwa kwa wakati na kwa ufanisi.

Kuzuia tatizo la kukojoa kitandani

  • Kupata usingizi mzuri na kwenda chooni mara kwa mara, usiku na mchana, kutasaidia kupunguza uwezekano wa kukojoa kitandani.

Vyanzo

https://medlineplus.gov/ency/patientinstructions/000703.htm#:~:text=The%20problem%20usually%20goes%20away,children%20who%20wet%20the%20bed.

Shares:
Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *