Kupima Mzingo wa Mkono
Kupima mzingo wa mkono ni utaratibu wa kupima mzingo wa kati wa sehemu ya juu ya mkono (MUAC) wa kushoto – ni kipimo cha ukubwa wa misuli ya mkono kinachotumika kujua hali ya lishe kwa watoto wenye umri zaidi ya miezi sita na watu wazima. Kipimo hiki hutumika kugundua utapiamlo wa kadiri na mkali.
- Mzingo wa kati wa sehemu ya juu ya mkono ukiwa kati ya sentimeta 11.5 -12.5 unaonesha Utapiamlo wa kadiri.
- Kipimo cha MUAC kikiwa chini ya sm 11.5 kinaonesha utapiamlo mkali (kulingana na miongozo ya WHO.
Kwa mujibu wa Shirika la Afya Duniani (WHO) upimaji wa mzingo wa kati wa sehemu ya juu ya mkono (MUAC) kwa watoto na watu wazima hufanyika kwa kuzingatia taratibu zifuatazo;
- Nawa mikono kwa maji safi na sabuni kabla na baada ya kumshika mteja. Endapo maji safi na sabuni hayapatikani, tumia dawa ya kuuwa vimelea vya magonjwa
- Ondoa nguo sehemu ya juu ya mkono wa kushoto wabega lake
- Kunja kiwiko cha mkono wa kushoto pembe ya nyuzi 90 huku kiganja cha mkono kikitazama juu
- Pima urefu wa mkono kutoka kwenye kifundo cha bega mpaka kwenye kiwiko, kisha tafuta katikati ya huo urefu na weka alama
- Mteja anyooshe mkono wake
- Zungusha utepe wa MUAC sehemu ya katikati ya mkono ulipoweka alama, usikaze wala kulegeza sana.
- Hakikisha namba za kwenye utepe zinasomeka
- Soma na kuandika vipimo vya MUAC kwa sentimita ya karibu ya desimali 0.1
Angalizo: Watoto wenye umri chini ya miezi 24 wapimwe wakiwa wamepakatwa na mzazi au mlezi