Maelezo ya jumla
Kupinda kwa mgongo (kibiongo) ni hali ya kupinda kwa uti wa mgongo kunakosababishwa na sababu mbalimbali. Kibiongo kinaweza kusababishwa na mkao usiofaa wa vijana wanaobalehe, kulika kwa mifupa wakati wa uzee, matatizo ya kano na tishu, uvimbe, au jeraha kwenye uti wa mgongo.
Wagonjwa wenye tatizo la Kupinda kwa mgongo hupatwa na uchovu, maumivu ya mgongo, na kukaza kwa misuli ya mgongo. Kwa hali kali sana, tatizo hili linaweza kuathiri moyo na mfumo wa upumuaji, na kusababisha shida kupumua au maumivu ya kifua. Picha za uti wa mgongo zinaweza kusaidia kutambua sababu ya shida hii. Matibabu na matarajio hutofautiana kati ya mtu na mtu, kulingana na sababu.
Ni zipi dalili za Kupinda kwa mgongo (kibiongo)?
Wagonjwa wenye tatizo la kibiongo wanaweza kupata dalili zifuatazo. Kadri tatizo linavyozidi kuendelea, wagonjwa wanaweza kuanza kuona dalili zinazohusisha mfumo wa upumuaji na moyo.
- Mwonekano wa kujikunja kwenda mbele / kibiongo
- Uchovu
- Maumivu ya mgongo
- Maumivu na kukaza kwa misuli ya mgongo
- Kupata shida kupumua
- Maumivu ya kifua
Ni nani yuko kwenye hatari zaidi ya kupinda kwa mgongo?
Watu wenye matatizo au hali zifuatazo wanaweza kuwa katika hatari zaidi ya kupata tatizo la Kupinda kwa mgongo :
- Kuwa na tatizo la udhaifu wa mifupa
- Kulika kwa gegedu za uti wa mgongo, kama unaotokana na ugonjwa wa yabisi kavu
- Ugonjwa unaosababisha kuvimba kwa gegedu na maungio ya uti wa mgongo ambao unaweza kupelekea kuungana kwa pingili za uti wa mgongo – Ankylosing spondylitis
- Tatizo la kano za mwili (connective tissue) kama vile ugonjwa wa Marfan – Marfan syndrome
- Ugonjwa wa kurithi unaosababisha misuli ya mwili kukosa nguvu na kusinyaa kadri muda unavyokwenda – Muscular dystrophy
- Ugonjwa wa kurithi unaosababisha kutokewa na vivimbe kwenye mfumo wa fahamu, mishipa ya fahamu, mgongo na ubongo – neurofibromatosis
- Ugonjwa wa mifupa unaotokana na mwili kushindwa kutengeneza vipande vipya vya mfupa ili kuchukua nafasi ya mifupa iliyochakaa – ugonjwa wa paget’s – Paget’s disease
- Ugonjwa wa polio
- Ugonjwa wa kifua kikuu unaoathiri uti wa mgongo
- Uvimbe kwenye uti wa mgongo
- Ugonjwa wa uti wa mgongo unatokana na uti wa mgongo kushindwa kutengenezwa vizuri wakati mtoto hajazaliwa / mgongo kubakia wazi – spina bifida
- Kupinda kwa uti wa mgongo kwenda upande mmoja – scoliosis
- Jeraha
- Mkao mbaya hasa kwa vijana wanaobalehe
Ni wakati gani unapaswa kutafuta msaada wa kitabibu?
Fika katika kituo cha afya ili kutambua sababu ya tatizo lako la Kupinda kwa mgongo (kibiongo)
Utambuzi
Sababu ya uchunguzi wa mwili ni kutambua sababu ya tatizo la kupinda kwa mgogngo.
- Daktari atachukua historia ya kitabibu na matibabu
- Daktari atakufanyia uchunguzi wa mwili
- Mwonekano: daktari atachunguza mgongo na kutafuta kama kuna matatizo yoyote
- Kubonyeza: daktari atagusa na kubinyabinya mgongo ili kuangalia kama kuna maumivu au mkazo wa misuli ya mgongo
- Atafanya kipimo cha kuangalia uwezo wa kujikunja – Adam’s forward bending test – Lengo la utaratibu huu ni kuangalia kama kuna tatizo kwenye uti wa mgongo. Wakati wa utaratibu huu, daktari atasimama nyuma ya mgonjwa na kumwomba ainamie mbele. Wagonjwa wenye tatizo la Kupinda kwa mgongo (kibiongo) wataonekana wamejikunja kama umbo la duara au mviringo.
- Kipimo cha eksirei au MRI: Picha za vipimo hivi, sio tu zinaweza kuonesha tatizo la mgongo, lakini zinaweza pia kusaidia kutambua sababu ya Kupinda kwa mgongo (kibiongo)
Uchaguzi wa matibabu ya kibiongo
Matibabu ya tatizo la Kupinda kwa mgongo (kibiongo) yanategemea sababu.
- Rekebisha mkao mbaya na lala katika godoro gumu. Marekebisho haya yanaweza kusaidia kwa wagonjwa wenye tatizo la Kupinda kwa mgongo (kibiongo) linalosababishwa na mkao mbaya
- Dawa: Dawa za kupunguza maumivu kama vile acetaminophen, ibuprofen au naproxen zinaweza kutumiwa kupunguza maumivu. Calcium +D zinaweza kupendekezwa kwa wazee wenye tatizo la udhaifu wa mifupa (osteoporosisi) linalosababisha Kupinda kwa mgongo (kibiongo). Dawa za antibiotiki zinapaswa kutumika kwa wagonjwa ambao tatizo la Kupinda kwa mgongo (kibiongo) limesababishwa na maambukizi. Dawa za tiba kemikali zinapaswa kutolewa kwa wagonjwa ambao kupinda mgongo kumesababishwa na saratani.
- Tiba mazoezi: Mtaalamu wa mazoezi anawafundisha wagonjwa mazoezi ya kuimarisha misuli ya mgongo. Aina hii ya tiba inaweza kusaidia kupunguza baadhi ya dalili.
- Upasuaji: Upasuaji unaweza kuhitajika kwa ajili ya tatizo la Kupinda kwa mgongo (kibiongo) kama kuna dalili za mfumo wa fahamu. Na, inaweza kuwa msaada kwa wagonjwa wenye tatizo la kupinda mgongo alilozaliwa nalo au saratani. Upasuaji unaweza kufikiriwa ia kama mgonjwa haitikii tiba ya dwa, au kama hali inazidi kuwa mbaya zaidi.
Kuzuia tatizo la Kupinda kwa mgongo (kibiongo)
Kuzuia tatizo la Kupinda kwa mgongo (kibiongo) kunategemea sababu. Kwa vijana wanaobalehe, kukaa mkao unaofaa ni muhimu sana.
Matarajio
Matarajio ya tatizo la Kupinda kwa mgongo (kibiongo) hutegemea:
- Sababu ya tatizo: Matarajio ya mgonjwa mwenye tatizo la Kupinda kwa mgongo (kibiongo) lililosababishwa na saratani huwa na matarajio mabaya ukilinganisha na sababu nyingine.
- Kama tatizo la mgonjwa limeambatana na matatizo mengine kama vile matatizo ya upumuaji, maumivu makali sana mgongo, matatizo ya mfumo wa fahamu na matatizo ya mgongo.