Maelezo ya jumla
Kutapika damu ni hali ya kutapika damu inayotoka sehemu ya mwanzo ya mfumo wa kumeng’enya chakula. Sehemu ya mwanzo ya mfumo wa kumeng’enya chakula inajumuisha tumbo, mdomo, koo, umio na sehemu ya mwanzo ya utumbo mdogo. Sababu za kutapika damu ni pamoja na uvimbe, kidonda, saratani na kupasuka kwa mishipa ya damu kunakosababishwa na kuharibika kwa ini/sirosisi. Dalili zinazoambatana ni pamoja na kichefuchefu, uchovu na kuchoka, kutokwa jasho, maumivu ya tumbo na mshtuko. Eksirei za kifua, Kipimo cha CT scan, kipimo cha ultrasound na kipimo cha endoscopy husaidia kufahamu mahali damu inapotokea. Matibabu ya kutapika damu yanategemea sababu. Lengo la mwanzo ni kuhakikisha damu inasimama au haiendelei kutoka ili uchunguzi zaidi ufanyike na matibabu kuanza. Matarajio ya tatizo la kutapika damu yanategemea sababu na kiasi cha damu iliyovuja.
Ni zipi dalili za kutapika damu?
Wagonjwa wanaweza kupata dalili zifuatazo:
- Kutapika damu
- Kichefuchefu
- Maumivu ya tumbo
- Uchovu na kuchoka
- Kutokwa jasho jingi
- Kupata kinyesi cheusi, kama lami
- Kushuka kwa shinikizo la damu
- Mshtuko
Matatizo mengine ya kiafya yanaweza pia kusababisha dalili hizi. Ni daktari pekee anayeweza kutofautisha. Mtu yeyote mwenye dalili hizi anapaswa kumwambia daktari ili tatizo lake litambuliwe na matibabu kuanza mapema
Ni zipi sababu za kutapika damu?
Zifuatazo ni sababu zinazoweza kusabisha kutapika damu:
- Umio
- Tumbo
- Vidonda vya tumbo
- Kukwanguliwa kwa tumbo – Gastric erosion
- Kuvimba kwa utando ute wa tumbo – Gastritis
- Kupasuka kwa mishipa ya damu kwa sababu ya kuongezeka shinikizo kulikosababishwa na kuharibika kwa ini – varices
- Saratani ya tumbo
- Uvimbe tumboni
- Sehemu ya mwanzo ya utumbo mdogo – duodenum
- Vidonda vya utumbo
- Kuvimba kwa utando ute wa utumbo – duodenitis
- Kuwepo kwa fistula kati ya mshipa mkuu wa aota na utumbo
- Ugonjwa wa ini
- Kuharibika kwa ini/sirosisi
- Saratani ya ini
Utambuzi wa kutapika damu
- Vipimo vya damu, kama vile vya kuangalia idadi ya seli zilizomo kwenye damu, uwezo wa damu kuganda, uwezo wa ini kufanya kazi, n.k.
- Eksirei ya kifua: Vipimo hivi huagizwa ili kuhakikisha kuwa hauna ugonjwa wa homa ya mapafu (nyumonia), maji kwenye mapafu, na kutoboka kwa umio
- Picha za CT scan na Picha za ultrasound zinaweza kuagizwa kuangalia kama mgonjwa ana ugonjwa wa ini, kuvimba kwa mfuko wa nyongo unaosababisha kuvuja damu, kuvimba kwa kongosho na kama kuna fitula ya aota na utumbo.
- Kipimo cha endoscopy: Kipimo hiki husaidia kuangalia ugonjwa ulipo kwenye umio, tumbo na sehemu ya mwanzo ya utumbo. Lakini pia, daktari anaweza kuzuia damu kuendelea kuvuja wakati wa kipimo hiki. Anaweza pia kuchukua tishu kidogo kutoka katika eneo lenye ugonjwa ili kuipima kwa darubini.
Ni wakati gani unapaswa kutafuta msaada wa kitabibu?
Fika kituo cha afya au idara ya dharura kama unatapika damu. Hali hii inahitaji matibabu ya dharura.
Uchaguzi wa matibabu ya kutapika damu
Matibabu ya kutapika damu yanategemea sababu. Leo la matibabu ni kurekebisha mshtuko na kusimamisha damu kutoka ili kuruhusu uchunguzi na matibabu kuendelea.
- Utaambiwa uache kula, utawekewa maji kwenye mishipa, na unaweza kuongezewa damu ili iwe kati ya 8 – 10g/dl kama itahitajika.
- Kupewa dawa aina ya PPI ni kawaida kwa mu mwenye kidonda kinachosababisha kuvuja damu, dawa hizi hutumika kupunguza kiwango cha asidi tumboni na kuongeza utengenezaji wa utete unaolinda tumbo na utumbo.
- Unaweza kufanyiwa endoscopy ili kuangalia damu inavujia wapi na ikiwezekana kuzuia damu inayovuja kwa kuchoma au kufunga sehemu inayovuja.
- Upasuaji unaweza kuhitajika kwa watu wanaoendelea kuvuja damu sana japo matibabu ya awali yamekwisha fanyika.
Kuzuia tatizo la kutapika damu
Kutibu ugonjwa uliopelekea kutapika damu ndio njia bora zaidi
Matarajio
Matarajio ya mtu baada ya kutapika damu hutegemea:
- Sababu iliyopelekea kutapika damu
- Kiasi cha damu uliyovuja au uliyotapika
- Hali ya mgonjwa kwa ujumla