Lishe ya vijana balehe
Lishe ya vijana balehe – Kijana balehe ni kijana mwenye umri wa kati ya miaka 10 hadi 19 ambapo mwanadamu anakua kwenye hatua ya ukuaji kutoka utotoni kuelekea utu uzima. Ni kipindi cha mpito katika makuzi ya kimwili, kiakili, kisaikolojia na maendeleo kiujumla. Upungufu wa virutubishi kwa vijana balehe wa kike una athari kubwa kwao. Hii inachangiwa na mabadiliko katika miili yao kama ukuaji wa haraka, kupoteza damu wakati wa hedhi na ulaji duni ambao husababisha upungufu wa virutubishi hasa madini chuma na vitamini B9 ijulikanayo kama asidi ya foliki. Ukuaji wa haraka unaotokea kwa kijana katika umri huu husababisha ongezeko la uhitaji wa nishati lishe na virutubishi vingine. Uhitaji wa virutubishi ni wa kiwango cha juu katika umri wa ujana ukilinganisha na umri wowote katika ukuaji wa mwanadamu. Lishe bora katika kipindi hiki ni muhimu sana.
Viashiria vya hatari vinavyoathiri afya ya kijana balehe
Utapiamlo katika umri huu huweza kuathiri kukomaa na kukua kwa via vya uzazi. Vilevile lishe bora ni muhimu katika umri huu ili kuzuia uwezekano wa kupata magonjwa sugu yasiyo ya kuambukiza wakati wa utu uzima kama vile magonjwa ya moyo, kisukari, shinikizo la juu la damu na saratani. Kuna sababu nyingi zinazochangia kudhoofisha lishe ya kijana balehe. Sababu hizo ni pamoja na mila na desturi au kukosekana kwa uhakika wa chakula chenye virutubishi vya kutosha. Sababu nyingine ni mimba za utotoni, magonjwa ya kuambukizwa na kutofanya mazoezi.
Madhara ya uzito uliozidi na kiribatumbo kwa vijana balehe
Utapiamlo wa uzito uliozidi na kiribatumbo husababisha athari za muda mfupi na athari za muda mrefu kwa vijana balehe. Kwa mfano;
- Kiwango cha juu cha sukari kwenye damu hivyo kusababisha madhara ya muda mrefu ya kisukari kisichokuwa cha kurithi (Aina ya pili ya kisukari)
- Kujifungua mtoto mwenye uzito mkubwa sana atapata ujauzito
- Husababisha kifafa cha mimba endapo kijana balehe atakuwa na uzito uliopitiliza kisha akapata ujauzito