Maelezo ya jumla
Mafua hali inayosababisha kutokwa na kamasi, kuziba kwa pua na kupiga chafya. Pia, unaweza kuwa na maumivu kooni, kikohozi, maumivu ya kichwa au dalili nyingine.
Dalili za mafua?
Dalili kwa kawaida hujitokeza ndani ya siku 2-3 baada ya kuambukizwa virusi, lakini wakati mwingine inaweza kuchukua mpaka wiki nzima kabla ya dalili kuonekana.
Dalili zinazowapata wagonjwa wengi ni:
- Kuziba kwa pua
- Kutokwa na kamasi
- Koo linalowasha au kukwaruza kwaruza
- Kupiga chafya
Watu wazima na watoto wenye mafua huwa na homa ya kadiri. Lakini watoto wachanga hupata homa kati ya 37.7-38.8 °C
Kulingana na virusi vilivyosababisha mafua yako, unaweza pia kuwa na dalili zifuatazo:
- Kikohozi
- Kupungua kwa hamu ya chakula
- Maumivu ya kichwa
- Maumivu ya misuli
- Maumivu ya koo
Ni nini husababisha mafua?
Mafua huwapata watu wengi sana kwa mwaka. Inawezekana utauugua ugonjwa huu mara nyingi zaidi kwa mwaka kuliko ugonjwa mwingine wowote. Mafua ndio sababu kuu ya utoro mashuleni na hata kazini. Wazazi mara nyingi hupata mafua baada ya kuambukizwa na watoto wao. Watoto kwa kawaida hupata ugonjwa huu mpaka mara nane kwa mwaka. Watoto huambukizwa na watoto wengine. Yanaweza kuenea kwa kasi kweli mashuleni. Mafua anaweza kutokea kipindi chochote lakini yanaongezeka zaidi wakati wa baridi au mvua.
Unaweza kupata mafua kama:
- Mtu mwenye mafua atapiga chafya, kukohoa au kupenga kamasi karibu yako
- Kama utagusa pua, macho au mdomo baada ya kugusa kitu chochote chenye virusi hivyo vinavyosababisha mafua, kama vile midoli au vitasa vya milango.
Ugonjwa huu unaambukiza zaidi siku 2-3 baada ya kuanza kwa dalili. Baada ya wiki mgonjwa hawezi kuambukiza tena.
Utambuzi wa mafua
Njia kuu ya kutambua kama una ugonjwa huu ni kupitia dalili zake, hii ni pamoja na: uchovu, kutokwa kamasi, kupiga chafya na kukohoa.
Hakuna njia ya maabara, njia ya picha au vipimo vingine vinavyohitajika kutambua mafua.
Kuna dalili zingine ambazo zinaweza kumsaidia daktari kutofautisha mafua na matatizo mengine, homa kali, kufadhaika sana na kikohozi chenye makohozi.
Uchaguzi wa matibabu ya mafua
Matibabu ni pamoja na:
- Kunywa maji mengi na kupumzika
- Kutumia madawa ya mafua
- Madawa ya mafua na kikohozi yanaweza kusaidia kupunguza makali ya dalili kwa watu wazima na watoto wakubwa. Hazisaidii kuponyesha ugonjwa huu, lakini zinakusaidia ujihisi vizuri.
- Madawa ya mafua na kikohozi hayashauriwi kutumiwa na watoto wenye umri chini ya miaka 6. Ongea na daktari kabla ya kumpa mwanao madawa ya aina hii. Hata kama maelekezo kwenye chupa yanasema ni ya watoto. Madawa haya mara nyingi hayawasaidii watoto wadogo na yanaweza kuwa na matokeo mabaya.
- Antibiotiki
- Madawa aina ya antibiotiki hayafai kutumika kutibu mafua. Hayasaidii na wakati mwingine yanaweza kuleta shida kubwa zaidi. Makamasi ya rangi ya njano au kijani huanza kuonekanan siku chache baada ya tatizo kuanza. Kama mafua hayatapona baada siku 10-14, daktari anaweza kuagiza utumie antibiotiki.
Tiba mbadala
Tiba mbadala ambazo hutumika, ni pamoja na:
- Supu ya kuku
- Supu ya kuku imekuwa ikitumika kutibu mafua kwa karne nyingi. Inaweza kukusaidia pia. Joto lake, maji maji yake na chumvi chumvi inaweza kukusaidia kupambana na maambukizi.
- Vitamini C
- Vitamini C hutumiwa na watu wengi kutibu tatizo hili. Tafiti zinaonesha haizuii mafua kwa watu wengi, lakini watu wanaotumia vitamin C mara kwa mara huwa na dalili za kawaida na vipindi vifupi vya ugonjwa huu. Kutumia Vitamini C baada ya kupata mafua haisaidii.
- Zinc
- Ukitumia virutuubisho vyenye zinc kwa angalau siku 5, inaweza kupunguza uwezekano wa kupata ugojwa huu. Ukitumia virutubisho vya zinc ndani ya masaa 24 baada ya kujihisi unaumwa, inaweza kupunguza ukali wa dalili na kupona haraka.
Kwa ujumla, tiba mbadala ni salama kwa watu wengi. Lakini, zingine zinaweza kusababisha athari mbaya au athari za mzio. Ongea na daktari kabla ya kujaribu tiba mbadala.
Wakati gani utafute matibabu haraka ukiwa na mafua?
Jaribu kutibu mafua yako nyumbani kwanza. Mwone daktari kama:
- Unaanza kupata shida kupumua
- Dalili zinazidi kuwa kali zaidi au hazipungui baada ya siku 7-10
Nini cha kutarajia?
Makamasi yanaweza kuongezeka na kuwa mazito na hata kubadilika rangi kuwa ya njano baada ya siku kadhaa. Hii ni hali ya kawaida na hauhitaji kutumia antibiotiki. Dalili nyingi kwa kawaida huisha baada ya wiki 1. Kama unajihisi kuumwa baada ya siku 7 mwone daktari ili atambue kama kuna tatizo jingine. Unaweza kuwa na maambukizi kwenye uwazi wa mfupa wa fuvu unaowasiliana na mianzi ya pua (sinusitis), mzio au tatizo jingine la kitabibu.
Matatizo yanayoweza kutokea
Mafua yanaweza kusababisha dalili za pumu kuongezeka kwa watoto wenye pumu.
Mafua yanaweza kupelekea mgonjwa kupata:
- Mkamba
- Maambukizi kwenye sikio
- Nyumonia
- Maambukizi kwenye uwazi wa mfupa wa fuvu unaowasiliana na mianzi ya pua-sinusitis
Nani yuko kwenye hatari zaidi?
Mafua yanaweza kuwaathiri watu wa jinsi, asili na rika zote.
Jinsi ya kuzuia
Ukifanya mambo haya matano utapunguza sana uwezekano wa kuugua mafua.
- Nawa mikono yako: Watoto na watu wazima wanapaswa kunawa mikono baada ya kupenga kamasi, baada ya kutoka chooni na kabla ya kula au kuandaa chakula.
- Safisha maeneo yanayoguswa na watu wengi mara kwa mara (kama vile handle za sink, vitasa vya milango, mouse za kompyuta n.k).
- Kama una mtoto, chagua daycare yenye watoto wachache. Daycare yenye watoto chini ya 7 hupunguza sana uwezekano wa kuambukizwa na kusambaa kwa vijidudu.
- Tumia vitakasa mikono ”sanitizer”: Bidhaa hizi hutumia pombe kuua vijidudu. Matone kidogo tu ya sanitizer yanaweza kuua 99.99% ya vijidudu bila maji.
Mfumo wa kinga ya mwili huusaidia mwili kupambana na maambukizi. Njia hizi sita huimarisha mfumo wa kinga ya mwili.
- Epuka kuvuta hewa yenye moshi wa sigara: Kaa mbali na watu wanaovuta sigara. Moshi wa sigara unasababisha matatizo mengi sana ikiwemo mafua.
- Epuka kutumia antibiotiki: Kutumia antibiotiki mara kwa mara kunaweza kusababisha usugu kwa dawa hizo. Ukitumia madawa mara kwa mara ndivyo na uwezekano wa kutokufanya kazi hapo baadae unavyoongezeka. Kwa hiyo siku za baadae utakapopata maambukizi itakuwa ngumu kuyatibu.
- Nyonyesha: Kumnyonyesha mtoto kunamkinga mtoto na magonjwa yanayoathiri mfumo wa upumuaji hata baada ya miaka kadhaa baada ya kuacha kunyonya. Watoto ambao hawanyonyeshwi, hupata maambukizi kwenye masikio mara tano zaidi ya walionyonyeshwa.
- Kunywa maji: Maji husaidia mfumo wako wa kinga kufanya kazi vizuri.
- Pata usingizi wa kutosha: Kutopata usingizi wa kutosha hukufanya uugue kwa urahisi.
MAELEZO ZAIDI KWA UFUPI KUHUSU MAFUA
Maelezo ya juma
Ni maambukizi ya sehemu ya juu ya mfumo wa hewa
Sababu ya mafua
Rhino virus ndio sababu kubwa ya mafua kwa watu wazima. Parainfluenza viruses, respiratory syncytial viruses, influenza na adenovirus wanasababisha mafua kwa watoto.
Epidemiolojia ya mafua
Mafua yanatokea kote duniani kwa makundi au kama mlipuko. Watu wengi wanapata mafua mara 1-6 kwa mwaka. Mafua yanawapata zaidi watu waoaishi nyanda za juu. Mafua anawapata zaidi watoto chini ya miaka 5 na taratibu huanza kupungua kadri umri unavyoongezeka.
Uambukizo wa mafua
- Moja kwa moja au kuvuta hewa yenye majimaji yaliyoruka wakati wa kuongea au kupiga chafya.
- Kwa kushika mikono au vifaa vyenye majimaji yaliyoka puani au koo la mtu mwenye maambukizi
Muda kabla dalili hazijaanza
Kati ya masaa 12 na siku 5, kwa hali ya kawaida masaa 48, inategemea na aina ya virusi
Muda wa uambukizo ya mafua
Masaa 24 kabla dalili kuanza mpaka siku 5 baada ya dalili kuanza
Nani yuko kwenye hatari zaidi
Watu wote wako kwenye hatari. Mafua kujirudia rudia huwa ni matokeo ya kuambukizwa na virusi mbalimbali
Dalili za mafua
- Kupiga chafya, kutokwa machozi, kujisikia vibaya kooni au kwenye pua, homa na uchovu
- Kukauka au maumivu ya koo
Utambuzi
Kwa kuangalia dalili na ishara
Matibabu ya mafua
Hakuna matibabu ya uhakika lakini unaweza
- Kupumzika
- Kujifukiza
- Kunywa maji na vinywaji kwa wingi
- Kutumia dawa za maumivu
- Kula mlo kamili
Kuzuia
- Elimisha jamii kuhusu umuhimu wa:
- Kuosha mikono
- Kufunika mdomo wakati wa kukohoa au kupiga chafya
- Kutupa tishu au vitambaa vya makamasi mahala salama
- Epuka maeneo ya msongamano hasa kama una mafua
- Kaa eneo lenye hewa ya kutosha