Maelezo ya jumla
Mafua ya nguruwe (Swine flu) ni ugonjwa unaosababishwa na virusi aina ya H1N1 na H3N2 wanaosababisha mafua. Dalili za mafua ya nguruwe zinafanana kabisa na zile za mafua ya kawaida.
Mwaka 2009 wanasayansi walitambua aina ya kirusi kinachoitwa H1N1. Kirusi hiki kilikuwa kimetengenezwa kwa muunganiko wa virusi ambao wanapatikana kwa nguruwe, ndege na wanadamu na kusababisha ugonjwa kwa wanadamu. Kati ya mwaka 2009 -2010, virusi wa H1N1 walisababisha ugonjwa wa mafua kwa watu wengi. Kwa sababu watu wengi sana duniani kote waliugua mafua haya, shirika la afya duniani lilitangaza ugonjwa huu kuwa janga la dunia. Ilipofika agosti mwaka 2010 WHO ilitangaza kuwa janga limedhibitiwa.
Siku hizi kuna chanjo ambayo inaweza kulinda watu dhidi ya mafua ya nguruwe yanayosababishwa na H1N1.
Dalili za mafua ya nguruwe
Ishara na dalili kuwa umeambukizwa virusi aina ya H1N1 vinavyosababisha mafua ya nguruwe zinafanana kabisa na dalili za mafua mengine ya kawaida, na hujumuisha:
- Homa, japo sio mara zote
- Kuhisi baridi
- Kikohozi
- Kuwashwa au maumivu kooni
- Kutokwa na kamasi au kuziba kwa pua
- Macho yanatoka machozi na mekundu
- Maumivu ya mwili
- Kichwa kuuma
- Uchovu
- Kuhara
- Kichefuchefu na kutapika
Dalili hizi zinaweza kuanza kuonekana siku moja mpaka tatu baada ya kukutana na virusi wa H1N1
Wakati gani umwone daktari
Sio lazima kumwona dakari kama una afya njema na ukapatwa na dalili na ishara za mafua kama homa, kukohoa au maumivu ya mwili. Lakini ni vizuri kumwona au kumpigia simu daktari wako kama una ujauzito au una ugonjwa wowote wa kudumu kama vile pumu, matatizo ya mapafu, kisukari au matatizo/magonjwa ya moyo kwa sababu uko kwenye hatarai zaidi ya kupata ugonjwa mkali na unawea ukapata matatizo
Sababu za mafua ya nguruwe
Virusi vya influenza aina ya H1N1 huathiri seli zinazofunika pua, koo na mapafu. Virusi wanaweza kuingia mwilini mwako kama utavuta hewa yenye majimaji yenye virusi hivyo baada ya mtu kukohoa au kupiga chafya au unaweza kupata baada ya kushika eneo lenye virusi hivyo na kisha ukashika macho , pua au mdomo. Hauwezi kuambukizwa Mafua ya nguruwe kwa kula nyama ya nguruwe.
Nani yuko kwenye hatari ya kupata mafua ya nguruwe
Kama unaishi eneo au unasafiri kwenda kwenye eneo lenye watu wengi walioambukizwa H1N1, unakuwa kwenye uwezekano mkubwa wa kuambukizwa.
Wakulima wanaofuga nguruwe na wataalamu wanaotibu au kushughulika na nguruwe nao pia wako kwenye hatari ya kukutana na mafua ya nguruwe kwa sababu wanafanya kazi kwa karibu sana na nguruwe.
Matatizo yanayoweza kutokea
Baadhi ya watu wanaopata mafua ya nguruwe, wanaweza kupata ugonjwa mkali na kupata matatizo, hii ni pamoja na:
- Kama una ugojwa wa moyo, pumu au magonjwa mengine ya kudumu, hali ako inaweza kuwa mbaya zaidi
- Nyumonia
- Unaweza kupata matatizo kwenye mfumo wako wa fahamu, unaweza kuchanganyikiwa na hata kupata degedege
- Unaweza kushindwa kupumua
Kuzuia mafua ya nguruwe
Kuna chanjo ya mafua ambayo inaweza kutolewa kwa watu wenye umi kuanzia miezi 6 na kuendelea. Kila mwaka inatengenezwa chanjo ya mafua ambayo inaweza kukinga watu dhidi ya virusi ambao wanaleta mafua kama vile H1N1 na H3N2. Chanjo ya mafua inaweza kupunguza hatari ya kupata mafua na kupunguza hatari ya kupata ugonjwa mkali wa mafua kama utaambukizwa. Chanjo inapunguza uwezekano wa mgonjwa kulazwa kwa sababu ya ugonjwa mkali.
Chanjo ya mafua ni muhimu hasa katika kipindi hiki cha mwaka 2020-21 kwa sababu ya uwepo wa ugonjwa wa homa kali ya virusi vya Corona (covid-19), ambao pia unasababisha dalili sawa na mafua. Ukipata chanjo ya mafua itapunguza dalili na itapunguza uwezekano wa kulazwa hospitalini. NB: Si rahisi kupata chanjo hii Afrika
Ukifanya mambo yafuatayo yatasaidia sana kupunguza uwezekano wa kupata mafua au kupunguza uwezekano wa mafua ya nguruwe kusambaa:
- Kaa nyumbani kama unaumwa. Kama una mafua, unaweza kuwaambukiza wengine. Kaa nyumbani kwa angalau masaa 24 baada ya homa yako kuisha.
- Nawa mikono yako vizuri mara kwa mara. Tumia sabuni na maji, au kama hakuna maji tumia vitakasa mikono (sanitizer)
- Funika mdomo wako unapokohoa au kupiga chafya. Kohoa au piga chafya kwa kutumia kitambaa au kwenye mkunjo wa kiwiko cha mkono na kisha nawa mikono
- Epuka kushikashika uso wako. Jitahidi usishike macho, pua au mdomo
- Safisha maeneo tanayoshikwa shikwa sana. Safisha mara kwa mara maeneo yanayoguswa sana, maeneo kama itasa, meza, remote za TV n.k, ili kupunguza uwezekano wa kushika eneo lenye virusi na kisha ukashika uso wako na kusababisha maambukizi
- Jitenge. Kaa mballi na mikusanyiko ya watu kwa kadri unavyoweza. Na ni vizuri kuepuka kukaa karibu na mtu ambaye anaumwa. Kama uko kwenye hatari kubwa ya kupata ugonjwa mkali unaotokana na mafua, kwa mfano kwa watu wenye umri chini ya miaka 5 au wazee zaidi ya miaka 65, au kama una ujauzito au kama una ugonjwa mwingine wa kudumu kama pumu – ni vizuri kuepuka kabisa mikusanyiko wakati wa mlipuko.