Maelezo ya jumla

Maumivu ya bega yanaweza kuwepo muda wote au yanaweza kuwepo unapoweka mkono katika mkao fulani au kuuchezesha kuelekea uelekeo fulani, kwa mfano unapouzungusha. Maumivu haya yanaweza pia kusambaa kuelekea kwenye mkono. Sababu za kawaida za maumivu ya bega ni kuvimba kwa misuli na kano ‘’tendons’’ zinazozunguka maungio ya bega. Maumivu ya aina hii yanaweza kutokea kama umetegua au kuvuta zaidi maungio, kwa mfano wakati wa michezo au kazi ngumu. Kadri maungio ya bega yanavyotumika kwa miaka mingi au kwa shughuli nyingi, ndivyo yanavyosagika, kulika na kuisha kwa sababu ya msuguano au sababu nyingine na mwishowe kusababisha maumivu ya bega.

Ukiwa na maumivu ya bega mwone daktari haraka kama

Ni vizuri kutafuta msaada wa kitabibu haraka kadri inavyowezekana kama una maumivu ya bega ambayo yanaambatana na mambo yafuatayo:

  • Maumivu makali au kuhisi uzito kifuani
  • Kutokwa jasho
  • Kupata shida kupumua
  • Kama una maumivu ya bega baada ya kuanguka au kuumia

Unachoweza kufanya wewe mwenyewe ukiwa na maumivu ya bega

Kuna mambo kadhaa unayoweza kufanya kupunguza maumivu na mkazo kwenye bega ili uanze kuchezesha mkono kama kawaida

  • Tumia dawa ya kupunguza maumivu. Madawa kama ‘’acetaminophen’’ au ‘’ibuprofen’’ yanapunguza maumivu. ‘’ibuprofen’’ inaweza pia kupunguza uvimbe na kusaidia kupunguza mkazo wa misuli
  • Unaweza kuweka barafu kwenye bega (unaweza kuchukua barafu iliotwangwa kwenye kifuko cha kubebea barafu na kisha ukaifunga na kitambaa chepesi ukaitumika) Shikilia barafu kwa dakika 10. Unaweza kurudia utaratibu huu mara 2-3 kwa siku 2 za mwanzo
  • Unaweza kutumia dawa za kuchua ‘’counterirritants’’, dawa za kuchua zinapooza mahali penye maumivu na kuongeza mzunguko wa damu wa maeneo hayo
  • Pumzisha bega kwa muda wa siku kadhaa, lakini hakikisha unapajongesha taratibu angalau kwa kunyanyua mambega taratibu mara kadhaa kwa siku. Kama usipopajongesha bega linaweza kukaza ukashindwa kulisogeza baadae ‘’bega lililoganda’’. Ukiona maumivu yanaanza kupungua, anza kufanya mazoezi ya bega.
    • Unaweza kufanya mazoezi yafuatayo mara 2 kwa siku ili kulegeza na kujongesha misuli. Unapaswa kuongeza kiwango cha mjongeo kadri maumivu yanapopungua
    • Weka mikono yako sawa na kisha inyanyue ukiwa umeinyoosha kwenda mbele mpaka utakapoanza kujisika vibaya. Irudishe taratibu mikono yako sawa. Rudia utaratibu huu mara 5

Maumivu ya bega

    • Weka mikono yako sawa na kisha anza kuinyanyua kwenda upande wa nje mpaka utakapoanza kujisikia vibaya. Irudishe taratibu mikono sawa. Rudia utaratibu huu mara 5
  • Wakati wa usiku, lalia upande ambao hauna maumivu na kumbatia mto ili kuutegemza mkono wenye shida. Ukilalia mgongo, kumbuka kuutegemeza mkono unaouma kwa mto
  • Hakikisha kuwa kwapa la mkono unaouma linakuwa safi na kavu ili kupunguza maumivu

Ukiwa na maumivu ya bega mwone daktari kama

Panga kumwona daktari:

  • Kama unaona maumivu ya bega yanazidi kuongezeka
  • Kama unaona maumivu hayapungui baada ya siku 2-3

Vyanzo

https://medlineplus.gov/ency/article/003171.htm

Shares:
Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *