Hatari za uvutaji wa sigara
- Uvutaji wa sigara huongeza uwezekano wa kupata magonjwa ya moyo. Baadhi ya bidhaa zinazotumika kutengeneza sigara husababisha kusinyaa na hata kuziba kwa mishipa ya damu, hali hii husababisha mshtuko wa moyo au kiharusi. Tafiti nyingi zinaonesha kuwa, watu chini ya miaka 40 wana uwezekano mkubwa wa kupata mshtuko wa moyo ikiwa wanavuta sigara.
- Uwezekano wa kupata mshtuko wa moyo huongezeka mara mbili zaidi kwa watu wanaovuta sigara pakiti nzima au zaidi kwa siku ikilinganishwa na wasiovuta.
- Timu ya wanasayansi wa Uingereza iliyoongozwa na Richard Doll ilifanya utafiti wa muda mrefu wa wataalam wa afya 34,439 kutoka 1951 hadi 2001. Uchunguzi huu ulionyesha kuwa uvutaji wa sigara hupunguza umri wa kuishi wa mvutaji kwa takribani miaka 10 na kwamba karibu nusu ya wavutaji wa sigara walikufa kutokana na magonjwa yanayosababishwa na uvutaji wa sigara (kansa, magonjwa ya moyo, na kiharusi).
- Watu wasiovuta sigara, wanakadiriwa kuishi miaka 5 hadi miaka 10 zaidi ya wanaovuta.
Hatari ya kuvuta hewa yenye moshi wa sigara
- Watu wanaovuta hewa yenye moshi wa sigara hata kama wao hawavuti sigara, huongeza hatari ya kupata magonjwa ya moyo kwa 25-30%.
- Uvutaji wa hewa yenye moshi wa sigara huongeza hatari ya kupata magonjwa ya mapafu, magonjwa ya moyo na aina fulani za kansa.
- Uvutaji wa hewa yenye moshi wa sigara kwa watu wasiovuta sigara, husababisha takribani vifo 3,000 kila mwaka vinavyotokana na saratani ya mapafu.
- Takribani watu 46,000 wanaoishi na watu wanaovuta sigara huvuta hewa yenye moshi wa sigara mara kwa mara, na wengi wao hufa kila mwaka kutokana na magonjwa ya moyo.
- Hata kiwango kidogo tu cha moshi wa sigara kwenye hewa huongeza maradufu hatari ya kupata magonjwa ya moyo. Kwa mujibu wa Ripoti ya Surgeon General ya mwaka 2006 , kuvuta hewa yenye moshi wa sigara hata kwa muda mfupi tu, husababisha chembe sahani kwenye damu kushikana kiurahisi na inaweza kusababisha mshtuko wa moyo au kiharusi.
Jinsi kuacha uvutaji wa sigara unavyopunguza hatari ya kupata magonjwa
Kuacha kuvuta sigara ni jambo la manufaa sana kwa afya yako na yawezekana baada ya muda fulani , baadhi ya madhara yaliyosababishwa na uvutaji wa sigara yanaweza kurekebika.
- Kuacha kuvuta sigara kwa muda wa mwaka 1 kunapunguza hatari yako ya kupata magonjwa ya moyo kwa 50% ikilinganishwa na mtu anayevuta.
- Hatari yako ya kupata kiharusi ni sawa na ile ya mtu ambaye hajawahi kuvuta kabisa sigara maishani mwake Miaka 5-15 baada ya kuacha kuvuta sigara.
- Miaka 10 baada ya kuacha kuvuta sigara, uwezekano wa kupata kansa ya mapafu, hupungua na kuwa sawa na wa mtu ambaye hawajawahi kuvuta kabisa sigara maishani. Miaka 15 baada ya kuacha kuvuta sigara, hatari yako ya kupata magonjwa ya moyo hupungua na kuwa sawa na mtu ambaye hajawahi kuvuta sigara.
Ninawezaje kuacha uvutaji wa sigara?
Hakuna njia moja ya kuacha kuvuta sigara inayomfaa kila mtu. Ili kuacha kuvuta sigara unapaswa kujiandaa kisaikolojia na kimwili. Ni lazima uamue mwenyewe kuwa unataka kuacha. Usiamue kuacha kwa sababu tu ya kutaka kuifurahisha.familia, marafiki, madaktarai au jamii. Weka mpango maalumu kabla ya kuacha kuvuta.
Mambo ya kuangalia kabla ya kuacha kuvuta sigara
Angalia vitu vilivyo kwenye orodha hii na weka tiki:
- _____ Chagua tarehe ya kuacha kuvuta sigara kisha uisimamie.
- _____ Andika sababu zako za kuacha kuvuta. Zisome kila siku kabla na baada ya kuacha kuvuta.
- _____ Andika ni kwa nini unavuta, unavuta wakati gani na huwa unavuta wakati gani? Fanya hivi ili kujifunza kama kuna vitu au hali maalumu zinazokufanya uvute.
- _____ Acha kuvuta sigara katika maeneo fulani (kama vile wakati ukiwa kazini au wakati wa chakula cha jioni), fanya hivi kabla ya kuacha rasmi kuvuta.
- _____ Tengeneza orodha ya shughuli unazoweza kufanya badala ya kuvuta sigara.
- _____ Anza kujitazama na kujichukulia kama mtu asiyevuta.
- _____ Waambie marafiki na familia yako kuhusu mpango wako wa kuacha kuvuta sigara. Unaweza kuwashawishi wanafamilia wengine wanaovuta waache pamoja nawe.
- _____ Muulize mtoaji wa huduma ya afya kama unaweza kutumia dawa au vifaa vya kukusaidia baada ya kuacha kuvuta, hii ni pamoja na gum, patches za nikotini, vidonge vya kuweka chini ya ulimi n.k.
- _____ Jiunge na kikundi cha msaada kinachowasaidia watu kuacha kuvuta sigara.
Mambo ya kuangalia baada ya kuacha kuvuta sigara
- Ondoa au tupa sigara zote.
- Ondoa au tupa vitu vyote vinavyohusiana na uvutaji wa sigara, kama vile majivu.
- Kama unaishi na mtu anayevuta sigara, muombe asivute sigara mbele yako au wakati ukiwepo. Ni vizuri ukimshawishi ajaribu kuacha kuvuta pamoja nawe.
- Usizingatie tamaa yako. Kumbuka kuwa hali hiyo unayojisikia ni ya muda mfupi na ujikumbushe ni kwanini unataka kuacha kuvuta.
- Kuwa busy na kazi! Pitia orodha yako ya shughuli unazoweza kufanya badala ya kuvuta sigara, fanya hizo.
- Unapopata hamu ya kuvuta sigara, vuta pumzi ndani. Ishikilie ndani kwa sekunde kama kumi na kisha iachie polepole. Rudia hili kwa mara kadhaa mpaka hamu ya kuvuta sigara itakapopita.
- Weka mikono yako busy. Chora, chezea penseli au majani au fanya kazi kwenye kompyuta.
- Badilisha shughuli au tabia ambazo zilihusiana na kuvuta sigara, kwa mfano badala ya kuchukua break ya kuvuta sigara, tembea au soma kitabu. .
- Kama unaweza, epuka sehemu au maeneo yenye watu wanaovuta sigara. Husiana na watu wasiovuta au nenda maeneo yasiyoruhusu mtu kuvuta sigara, kama vile majumba ya sinema, , majumba ya maonesho, maduka au maktaba.
- Usijaribu kutuliza hamu yako ya kuvuta sigara kwa kula chakula au kula vitu vyenye sukari nyingi. Kula vyakula vya afya kama vile karoti, pipi ngumu zisizo na sukari. au tafuna gum wakati hamu inapokujia ili kuzuia kuongezeka uzito.
- Kunywa maji mengi, lakini upunguze vileo na kahawa. vinaweza kusababisha hamu ya kuvuta kuongezeka.
- Jikumbushe kila wakati kwamba wewe si mvutaji. Watu wasiovuta hawavuti.
- Fanya mazoezi. Kufanya mazoezi kuna faida nyingi na yatakufanya u-relax
Utajisikiaje baada ya kuacha kuvuta sigara?
- Unaweza kuwa unatamani sana sigara, utakuwa na hasira, utahisi njaa sana, utakuwa ukikohoa mara kwa mara, utapata maumivu ya kichwa, utapata ugumu kuzingatia mambo na kufunga choo. Dalili hizi hutokea kwa sababu mwili wako umeizoea nikotini ambayo huwa kwenye sigara.
- Kwa wiki mbili baada ya kuacha kuvuta sigara, utapata dalili hizi zinazotokana na kuacha kuvuta sigara, jaribu kujisimamia. Jifikirie ni kwa sababu gani umeamua kuacha. Jitie moyo, kwa sababu hizo ni ishara kuwa mwili wako unapona na unazoea kuishi bila sigara.
- Dalili hizi zinazotokana na kuacha kuvuta sigara ni za muda tu. Dalili hizi ni kali zaidi baada tu ya kuacha kuvuta na hupungua na kuisha kabisa baada ya siku 10 mpaka 14. Kumbuka kuwa dalili hizi zinazotokana na kuacha kuvuta ni rahisi kutibika kuliko magonjwa yanayotokana na kuvuta sigara.
- Bado unaweza kuwa na hamu ya kuvuta sigara. Mazingira na watu unaokutana nao wanaweza kuwa kishawishi kikubwa cha kuanza tena kuvuta sigara. Njia bora ya kushinda vishawishi hivi ni kuvikabili na kujizuia kuvuta.
Ni nini kitatokea baada ya kuacha kuvuta sigara
Baada ya dakika 20
- Unaacha kuchafua hewa
- Shinikizo lako la damu na mapigo ya mojo hupungua
- Joto la mikono na miguu yako huongezeka
Baada ya masaa 8
- Kiwango cha kaboni diokisaidi ndani ya damu hurudi na kuwa cha kawaida.
- Viwango vya oksijeni katika damu yako huongezeka
Baada ya masaa 24
- Hatari yako ya mshtuko wa moyo hupungua
baada ya masaa 48
- Mishipa ya fahamu huanza kuzoea ukosefu wa nikotini mwilini.
- Uwezo wako wa kuonja na kunusa unaanza kurudi
Baada ya wiki 2 hadi miezi 3
- Mzunguko wako wa damu unaboreka
- Uwezo wako wa kuhimili mazoezi unaboreka
Baada ya miezi 1 – 9
- Kukohoa, kuziba kwa pua, uchovu na matatizo ya upumuaji yanapungua
- Kiwango chako cha nguvu kwa ujumla huongezeka
Baada ya mwaka 1
- Hatari yako ya kupata ugonjwa wa moyo inapungua kwa 50% tofauti na mtu anayevuta.
Baada ya miaka 5 – 15
- Hatari yako ya kupata kiharusi inapungua sana mpaka kuwa sawa na watu ambao hawajawahi kuvuta kabisa.
Baada ya miaka 10
- Hatari yako ya kufa kutokana na saratani ya mapafu inapungua sana na kuwa sawa na mtu ambaye hajawahi kuvuta hata mara moja maishani mwake.
- Unapunguza aina nyingine za saratani kama vile – za mdomo, koromeo, kimeo, kibofu cha mkojo, figo na kongosho
Baada ya miaka 15
- Hatari yako ya kupata ugonjwa wa moyo inapunguzua na kuwa sawa na watu ambao hawajawahi kuvuta kabisa.
Ikiwa utavuta sigara tena (hii inaitwa relapse) usipoteze tumaini. 75% ya watu wanaoacha hurudia tena kuvuta sigara. Wengi wao huacha kuvuta sigara angalau mara tatu kabla ya kufanikiwa kuacha kabisa. Kama ukirudia kuvuta usipoteze tumaini, usife moyo, pitia sababu zako za kutaka kuacha. Kisha panga tena mpango wa kuacha na nini ufanye utakapopata hamu ya kuvuta tena.
Vyanzo
https://medlineplus.gov/smoking.html#:~:text=Smoking%20can%20damage%20your%20blood,Vision%20problems